MICHEZO MEI MOSI IRINGA YAZINDULIWA


KAMATI ya mashindano ya Mei Mosi Taifa imesikitishwa na kupungua kwa timu shiriki katika mashindano ambayo yamezinduliwa leo uwanja wa Samora na Mgeni rasmi Mkuu wa Mkoa wa Iringa Mhe. Amina Juma Masenza.

Kauli hiyo imetolewa na makamu mwenyekiti wa kamati ya michezo ya Mei Mosi Kitaifa Joyce Benjamini wakati wa uzinduzi wa michezo ya Mei Mosi kwenye kiwanja cha kumbukumbu ya Samora Mkoani Iringa ambapo amesema timu zimepungua kutoka timu kumi na Tano (15) mwaka jana hadi timu kumi (10) mwaka huu wa 2018.

Benjamini alisema kuwa kupungua kwa idadi ya timu shiriki kunatokana na baadhi ya mashirika ya sekta za UMMA na Serikali kushindwa kupeleka timu kwa visingizio vya ukata ili hali timu ya Rais ikiwa imeshiriki mashindaano hayo.

“Mheshimiwa Mkuu wa Mkoa tunapenda kutoa malalamiko yetu juu ya kupungua kwa hizi timu na kusingizia ukata wa pesa jambo ambalo sio kweli kwa kuwa Waziri Mkuu, Makamu wa Rais na Rais wetu ni viongozi wapenda michezo hivyo uoga wao ndio umefanya kushindwa kuzileta timu zao zishiriki mashindano haya”.  Alisema  Benjamini

Benjamini alisema kuwa hakuna mahali ambako Rais amekataza wafanyakazi wa Serikalini kutoshiriki michezo mbalimbali, viongozi wetu wa serikali wamekuwa waoga kwenye matumizi ya fedha za Serikali, anachokitaka Rais ni uhalisia wa matumizi ya fedha katika maeneo husika.

“Mheshimiwa Mkuu wa Mkoa hata ukiangalia kwenye Ilani ya Chama Cha Mapinduzi ya mwaka 2015 hadi mwaka 20102 ibara ya 61 ukurasa wa 218 hadi 219 unasema wajuu ya kuinua na kuendeleza michezo hapa nchini,sasa kwanini Viongozi hawafuati Ilani hiyo”.  Alisema Benjamini.

Benjamini alizitaja timu zinazoshiriki mashindano hayo Mkoani Iringa kuwa ni timu kutoka Ofisi ya Rais –Ikulu,Wizara ya Uchukuzi, Chuo Kikuu kishiriki cha Afya na sayansi (MUHAS), Hifadhi za Ngorongoro, Geita gold mine (GGM), Mamlaka ya mapato Tanzania (TRA),Shirika la umeme Tanzania (TANESCO), Tumbaku-TTPL ya Morogoro, Ukaguzi na Wenyeji timu ya RAS Iringa.

Naye Mgeni rasmi Mkuu wa Mkoa wa Iringa Amina Masenza aliyewakilishwa na Afisa Elimu Mkoa wa Iringa Majuto Njanga amezionya timu ambazo zinashiriki kwenye Michuano ya Mei Mosi kuacha kuchukua wachezaji ambao sio wafanyakazi kwani kufanya hivyo kunapunguza ladha ya mashindano hayo.                                

Njanga amesema kuwa michezo hujenga undugu na furaha baina ya wanamichezo hivyo kuwaingiza wachezaji ambao sio wafanyakazi kwenye mashindano hayo wataondoa maana halisi ya mashindano hayo jambo ambalo linaweza kuwafanya kushindwa kufikia malengo yao waliojiwekea. 

“Mashindano haya ni ya wanamichezo wafanyakazi,kuna wale wanamichezo ambao sio wafanyakazi ambao wanajulikana kama mamluki au wavamizi kwamba hapa sio mahala pao nawasihi tuchezeshe wafanyakazi halisi ili mshindi apatikane kihalali na sio vyenginevyo kwa sababu ni hatari sana kumleta mwanamichezo ambaye sio mfanyakazi kwenye michezo hii anaweza kuvunjika mguu au akifa kwa mfano hatuombei itokee hiyo itakuwaje “Alisema Njanga


Aidha Njanga alizitaka timu hizo kuacha kuwatumia wachezaji wa aina hiyo kwani wana madhara makubwa hasa pale yanapokuwa yakijitokeza kwa kuzitaka timu zenye utamaduni huo kuhakikisha wanaondokana nao. 

Akizungumzia waamuzi wanaochezesha mashindano hayo, Njanga aliwataka kuchezesha kwa haki bila upendeleo kwa kufuata sheria za mchezo husika ili mshindi aweze kupatikana kihalali kwa sababu wakienda kunyume chake wanaweza kusababisha tafrani na manung’uniko kwa baadhi ya timu shiriki. 

Hali kadhalika aliwataka kuhakikisha wanakuwa na nidhamu ya hali ya juu wakati wote wa mashindano ikiwemo kukubaliana na matokeo pindi watakapojikuta wamefungwa wakati wa mashindano hayo.

Baadae Njanga alikagua timu zilizokuwepo uwanjani wakati wa uzinduzi wa michuano hiyo ambayo inatarajiwa kufikia kikomo Tarehe 29 Mwezi huu na kwa washindi kupewa zawadi na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dr. John Pombe Magufuli siku ya Mei Mosi ambapo atakuwa Mgeni Rasmi.


MATUKIO KATIKA PICHA WAKATI WA UZINDUZI HUO











 MGENI RASMI AKIZUNGUMZA 


Share on Google Plus
Ahsante kwa kutembelea site yangu, unaweza kunicheki kwenye mitandao ya kijamii kwa kubonyeza icons juu kulia na kunipata moja kwa moja kwenye Facebook, Twitter na Instagram...Endelea kuwa karibu yangu ili uweze kufikiwa na chochote kinachonifika.
    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 Maoni:

Post a Comment