VIJANA Mkoani Kilimanjaro
wametakiwa kuchangamkia fursa ya mikopo ya asilimia kumi ambayo imekuwa
ikitolewa na Halmashauri mbalimbali nchini kwaajili ya kujikwamua kiuchumi
kupitia mikopo hiyo isiyokuwa na riba.
Wito huo umetolewa leo Aprili 14, 2026 Bungeni
jijini Dodoma na Mbunge wa viti Maalumu Mkoani Kilimanjaro Mheshimiwa Zuena
Bushiri wakati akichangia hotuba ya bajeti ya Waziri Mkuu.
Mbunge huyo amesema kuwa
mnamo mwezi Februari 2026, Serikali ilitoa kiasi cha shilingi bilioni 200
kwaajili ya mikopo ya vijana ikiwa ni jitihada za Rais Samia katika kuwakwamua
vijana kiuchumi waweze kufanya biashara zao na kusaidia familia zao.
Ameishauri Serikali
kupitia mikopo hiyo kusimamia vizuri utaratibu wa utoaji wa mikopo hiyo ili
ikatumike kwa lengo lililokusudiwa ili vijana waweze kunufaika ipasavyo.
Katika mikopo ya asilimia
kumi inayotolewa na Halmashauri nchini, Mbunge Zuena amesema zipo baadhi ya
changamoto ikiwemo ujazaji wa dodoso, akisema wapo baadhi ya watu wamekuwa
wakishindwa kujaza madodoso hayo wakiwemo wananchi wa vijijini.
Amesema asilimia kubwa ya
mikopo hiyo ambayo imekuwa ikiwalenga akina mama wa vijijini ambao hawawezi
kufanya biashara kubwa, maafisa maendeleo ya jamii wamekuwa wakiwatuma na
kuwaambia wakajaze dodoso jambo ambalo hawawezi na matokeo yake wamekuwa
wakienda kwenye huduma za Stationery ambako hutozwa fedha.
Ameishauri Serikali
kusimamia vizuri swala hilo kwa kuwatoa maafisa maendeleo ya jamii na kata
maofisini na kushuka chini kwa wananchi kwa makundi yote ili wawasaidie waweze
kupata fedha hizo za mikopo iwasaidie kwenye biashara zao.
Awali akichangia Hotuba
ya Waziri Mkuu, Mheshimiwa Zuena aliipongeza Serikali kwa kuwajali wananchi
wake kwa kupiga hatua kubwa kwenye maswala ya Afya kuanzia ngazi ya Kata hadi
kanda.
Amewataka wananchi
kumpongeza Rais Samia Suluhu Hassan kwa kuboresha sekta ya Afya nchini akisema
hotuba hiyo inaonyesha kuwa mwaka 2024 Taifa lilikuwa na vituo vya kutolewa
huduma za afya kwa asilimia 80 na kwamba hadi mwezi Februari 2026 wastani wa
utoaji huduma ni asimilia 89 akisema ni hatua kubwa imepigwa na Serikali.
Amempongeza Rais Samia
kwa kuhakikisha huduma za kibingwa na bobezi zinapatikana nchini ikiwa awali
wananchi wengi walilazimika kusafiri kwenda nchi za nje hasa India kwaajili ya
kutafuta matibabu na vipimo ambavyo kwasasa vinapatikana nchini akitolea mfano
wa kipimo cha Ugonjwa wa Saratani na huduma ya upandikizaji wa figo ambayo
inapatikana Hospitali ya Taifa Muhimbili na Benjamin Mkapa Dar Es Salaam.
Ameishauri Serikali
kuongeza ajira ya watumishi kwenye kada ya afya ili iendane na idadi ya vituo
vya kutolea huduma sanjari na kuiomba Serikali kushusha huduma ya tiba mtandao
kuanzia Hospitali za Rufaa hadi za Wilaya.
Ahsante kwa kutembelea site yangu, unaweza kunicheki kwenye mitandao ya kijamii kwa kubonyeza icons juu kulia na kunipata moja kwa moja kwenye Facebook, Twitter na Instagram...Endelea kuwa karibu yangu ili uweze kufikiwa na chochote kinachonifika.



0 Maoni:
Post a Comment